Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko amesema tayari mtambo namba nane kutoka kwenye Mradi wa kufua umeme wa Julius Nyerere umekamilika na sasa unaingiza megawati 235 kwenye gridi ya taifa.
Dkt Biteko ametoa taarifa hiyo wakati akizindua taarifa za utendaji katika Sekta ndogo ya Umeme, Gesi Asilia na Mafuta kwa mwaka 2022/2023 jijini Dodoma ambapo amesema kwa sasa Jumla ya megawati 470 zinazalishwa kutoka JNHPP na tayari zimeingizwa kwenye gridi ya taifa.
Kuhusu sekta binafsi amesema, “Sekta binafsi imetutoa kimasomaso, Serikali haiwezi kufanya kila kitu, wamefanya kazi kubwa mno kwenye mafuta, gesi na hata kwenye uzalishaji umeme, wito wangu kwenu msibaki nyuma changamkieni fursa, na kwa taasisi zilizo chini ya Wizara msione sekta binafsi kama watu wajanjawajanja, tuwape kipaumbele.” Amesema Dkt. Biteko
Akitoa taarifa za utendaji katika Sekta ya Nishati, Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Dkt. James Andilile alisema kuwa Sekta ya Nishati inaendelea kuimarika ikiwemo uwekezaji kwenye miundombinu ya
umeme uwekezaji umeongezeka katika uzalishaji, usafirishaji na usambazaji, upotevu wa umeme unazidi kupungua na kubainisha wateja wa umeme wameongezeka kutoka milioni 3.8 mwaka 2021/22 hadi milioni 4.4 mwaka 2022/2023.
