Na Mwandishi wetu - Kibondo
Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Kibondo mkoani Kigoma Bw. Diocles Rutema amewaagiza maafisa watendaji wa kata kwa kushirikiana na madiwani, kuhakikishe watoto ambao hawajaripoti shuleni watafutwe na ijulikane mahali walipo.
Wanafunzi ambao wamefaulu na kupangiwa kuripoti kuanza masomo ya kidato cha kwanza kwa mwaka huu 2026 katika halmashauri ya wilaya Kibondo ni wanafunzi 3450 na ambao hawajaripoti hadi kufikia Februari 11 ni wanafunzi 189 pekee sawa na asilimia 6 tofauti na miaka iliyopita ambapo mkurugenzi mtendaji Diocles Rutema kupitia kikao cha baraza la madiwani cha kupokea na kujadili taarifa za shughuli zilizofanyika kwa robo ya pili kwa mwaka wa fedha 2025,2026 amezipongeza kata ambazo wanafunzi wote wamesharipoti shuleni ambazo ni Misezero, Itaba, Murungu na Kitahana
Rutema amesema shule ambazo wanafunzi wote hawajaripoti wafuatiliwe na waende shuleni ikiwemo Biturana, Kigina, Muramba na Kisogwe na wanafuzi hao wajulikane walipo kama aidha wanasoma katika shule za binafsi au wapo mtaani lengo likiwa ni kufikia asilimia 100 ya watoto wote kuripoti shuleni
Mwenyekiti wa Chama cha mapinduzi CCM wilaya ya Kibondo Hamis Tahiro amepongeza jitihada hizo huku mwenyekiti wa chama cha ACT wazalendo Nicholaus Kilunga akieleza kuwa changamoto ndogondogo zikiwemo za madawati ziendelee kutafutiwa ufumbuzi
Akifunga kikao hicho mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Kibondo ambaye ni diwani wa kata Kibondo mjini Bw. Alex Baragomwa amewataka madiwani kuendeleza ushirikiano ili kutimiza mahitaji ya wananchi.




